KUANZISHA BIASHARA YAKO, MAMBO YA MSINGI. | JIFUNZE UJASIRIAMALI

KUANZISHA BIASHARA YAKO, MAMBO YA MSINGI.



Kuanzisha biashara mpya ni jambo linalohitaji maandalizi, hata hivyo kiwango cha  maandalizi kitatofautiana  kulingana na mambo mbalimbali yakiwemo ukubwa wa biashara yenyewe, kiasi cha mtaji, aina ya biashara, mazingira ya biashara nk. Katika makala hii tutaegemea zaidi upande wa zile biashara ndogondogo ambazo wengi wa watu hapa kwetu ndio huzifanya.

Kama tulivyotangulia kusema, mambo ya msingi au kwa maana nyingine hatua zinazopaswa kufuata wakati wa kuanzisha biashara ndogo hayatofautiani sana na yale mtu anapotaka kuanzisha biashara kubwa;

UTAFITI
Baada ya kufanya maamuzi ni biashara gani unayotaka kuanzisha , kama ni bidhaa au huduma, sasa chunguza maswala mbalimbali kama vile, eneo biashara itakapokuwa, wateja, soko, mfumo wa biashara kisheria ikiwa ni mtu binafsi, ubia au kampuni, nk. Katika utafiti unaweza ukapata majibu mengi kwa swali moja lakini unachotafuta hapa ni jibu moja tu au mawili katika kuandaa mpango wa biashara hatua inayofuata.



MPANGO.
Hatua nyingine na iliyokuwa muhimu sana ni mpango wa biashara yako. Mpango wa biashara ni majumuisho ya utafiti uliofanya , hapa sasa ndio unapoamua ni njia zipi au mikakati ipi uitumie baada ya kufanya utafiti. Madhalani uligundua aina mbili za bidhaa unazoweza kuuza, chagua moja inayofaa zaidi na upange kuwa ndiyo utakayoiuza. Mpango/mchanganuo wa biashara unaweza ukauweka kichwani tu, lakini unakuwa na maana na manufaa zaidi unapoandikwa kwenye karatasi.

SUALA LA FEDHA.
Kutafuta fedha kwa ajili ya kuanzia pia ni hatua muhimu kabla haujaanza kufanya biashara. Kuna njia kadhaa na moja, unaweza kupata mtaji kutokana na akiba yako mwenyewe uliyodunduliza kutokana na vyanzo mbalimbali kama vile, mshahara, urithi, zawadi, faida ya biashara nyingine nk. Njia ya pili, ni mkopo kutoka kwa aidha ndugu jamaa na marafiki au taasisi mbalimbali za fedha zikiwemo benki na saccos.

MAANDALIZI YA SEHEMU YA BIASHARA.
Eneo biashara itakapokuwa panaweza pakawa ni duka, ofisi ama eneo lolote lile biiashara itakapofanyika. Utahitaji leseni na vibali mbalimbali kulingana na aina na ukubwa wa  biashara yenyewe. Biashara nyingine ndogo sana hazihitaji  vibali vingi na wakati mwingine hauhitaji kuwa na leseni wala kibali chochote kile. Utahitaji pia kuwa na bidhaa au huduma unazotarajia kuuza, vifaa mbalimbali kama vile, ofisi,simu, kompyuta, fax na vitabu vya kumbukumbu na hesabu za biashara yako.

UENDESHAJI.
Uendeshaji wa biashara yako utategemea sana Mpango wako wa biashara ulivyouandaa, iwe umeuhifadhi kichwani au hata umeuandika kwenye karatasi. Katika hatua hii utatakiwa upange bei ya bidhaa/huduma zako, kuweka mfumo wa kumbukumbu na hesabu wa biashara, kupanga masaa ya kazi, kutafuta masoko, kampeni za matangazo nk. Yoote hayo itakubidi ufuate mpangilio wako wa biashara huku ukifanya marekebisho pale hali halisi inapokuwa tofauti na ulivyopanga kwani Mpango ni Dira, hauwezi ukalingana mia kwa mia na hali halisi.


KUAJIRI.

Inawezekana wewe mwenyewe ndiyo kila kitu, Mkurugenzi, Meneja, Sekretari na hata Mesenja ni wewe mwenyewe, lakini kumbuka ni lazima tu utafika wakati biashara ikipanuka utahitaji kuajiri wasaidizi. Kabla haujamuajiri mtu kwanza pima ikiwa hatua hiyo itakuwa na manufaa kwako au la. Mchunguze unayetaka kumuajiri, fanya naye mahojiano kufahamu historia yake vizuri ikiwa ni pamoja na wewe mwenyewe kuzingatia sheria na taratibu za  nchi  kama vile kutokuajiri watoto wadogo nk.

0 Response to "KUANZISHA BIASHARA YAKO, MAMBO YA MSINGI."

Post a Comment