ENEO LA BIASHARA YA DUKA LA NGUO REJAREJA, JE NIFUNGUE MJINI AU KIJIJINI?-MWANAFUNZI WA KIKE CHUO KIKUU | JIFUNZE UJASIRIAMALI

ENEO LA BIASHARA YA DUKA LA NGUO REJAREJA, JE NIFUNGUE MJINI AU KIJIJINI?-MWANAFUNZI WA KIKE CHUO KIKUU

Mwanafunzi wa chuo anayetaka kuanzisha biashara angali chuoni

Ni siku chache zimepita tangu msichana mmoja, mwanafunzi wa kike katika chuo kimoja huko kanda ya ziwa anipigie simu akiomba ushauri ikiwa kama anaweza kufanya biashara ya duka la nguo rejareja akiwa bado anaendelea na masomo yake chuoni.

Katika kazi hii ya uandishi mara nyingi nimekukutana na maswali hasa ya vijana wanafunzi wa vyuo wenye nia na shauku ya kutaka kuanzisha biashara wangali bado wanasoma na jambo moja lililonistaajabisha sana ni kugundua karibu wanafunzi hao wote wana tabia moja inayofanana utafikiri huambiana kabla ya kuuliza maswali yao, nitakwenda kuielezea tabia hiyo ya ajabu hivi punde tu endelea kusoma.....

Mwanafunzi huyo wa kike wa chuo sitaweza kumtaja kwa majina yake halisi wala utambulisho wake mwingine wowote ule kwani hajanipa ruksa na badala yake hapa nitamuita tu kwa jina bandia la Katarina.

Katarina alitaka kujua ni mbinu na mikakati ipi ambayo anaweza kuitumia ili biashara hiyo ya nguo iweze kuendelea na kushamiri pasipo yeye kuwa pale muda wote wala kuathiri muda wake wa masomo chuoni.

Na mimi kama nilivyokwishawahi siku za nyuma kutoa majibu kwa vijana wengine mbalimbali hapa, nilimwambia hilo ni jambo linalowezekana kabisa lakini ni sharti ahakikishe anampata msaidizi mwaminifu atakayekuwa akifanya kazi ya mauzo dukani.

Kwa kuwa duka la kuuza nguo rejareja ndio lilikuwa wazo lake la kwanza, niliendelea kumsisitizia pia umuhimu wa matumizi ya mbinu na mifumo ya uthibiti wa mapato ya duka la rejareja iliyoelezwa katika kitabu cha MAFANIKIO YA BIASHARA YA DUKA LA REJAREJATOLEO LA 2025 & GENGE na kabla hata sijamaliza Katarina akaniambia, “Nataka hicho kitabu ili niweze kujifunza hiyo mifumo nikiwa nimetulia na kuchagua nitumie upi kwenye biashara yangu ya nguo


muamala wa manunuzi ya kitabu cha duka la rejareja

Hakusita akalipia shilingi elfu 10 chapchap kama uonavyo muamala aliotuma hapo juu baada ya kukosea namba kidogo nikatuma upya, na mimi nikamtumia kitabu chake. Zilipita kama siku mbili hivi akiwa anakisoma na kisha nikaona tena namba ya simu yake ikiita.

Hapa sasa ndipo utapata lile jibu la swali nililoahidi nitalijibu baadae, kwamba ni tabia gani ya kushangaza wanafunzi wote wa chuo wanaotaka kuanzisha biashara wangali bado chuoni wanayo pasipo hata wao wenyewe kujua kama wanayo.

Karibu wanafunzi wote wa vyuo wanaonipigia simu ama kutuma ujumbe mfupi wakitaka niwashauri juu ya kuanzisha biashara wangali bado chuoni wakisoma wana tabia moja inayofanana, huwa hawaulizi swali moja na kuishia hapo.

Watarudi tena na tena kuuliza kiasi kwamba ikiwa wewe ni mtu usiyependa usumbufu unaweza kuwablock au kuonyesha kukereka.

Lakini binafsi yangu mimi tabia yao hii hainikeri bali inazidi kunitia hamasa zaidi na ari ya kuwasaidia ninapokumbuka namimi pia kuna nyakati nilikuwa napitia kipindi kama chakwao na jinsi nilivyokuwa natamani kudadisi masuala ya biashara au ubunifu mwingine wowote ule wa kuleta maendeleo. Naona fahari kuwaonyesha njia sahihi ili siku moja wafanikiwe maishani.

Nakumbuka kuna mwanafunzi mmoja aliyekuwa akifuatilia masomo yangu kwa email kipindi fulani akiwa anasoma sekondari, akawa ananipigia simu kutaka ushauri kwangu. Aliendelea kunisumbua na maswali hata pale alipoingia chuo kikuu akiniambia bado hana uiwezo wa kulipia vitabu au course zangu za uandishi wa michanganuo.

Hata hivyo na mimi sikukata tamaa wala kuacha kumtumia masomo kwa email. Kijana yule alipokuja kuhitimu Chuo kikuu alikuja kugeuka kuwa mteja wangu mkubwa akinunua karibu vitabu vyangu vyote na semina, na mpaka sasa hivi ninapoandika hapa ni muajiriwa mahali fulani lakini kando akimiliki miradi kadhaa ya kiuchumi inayomuingizia kipato kizuri cha ziada.

Tukirudi tena kwa Katarina aliponipigia simu kwa mara ya pili, safari hii alitaka nimshauri jambo jingine. Katika mawazo ya biashara alizokuwa amefikiria kuanzisha mbali na biashara ya duka la kuuza nguo rejareja, alikuwa na wazo jingine mbadala ikitokea la nguo akaliacha, la kuanzisha biashara ya miamala ya simu, kutoa na kuweka pesa kupitia Tigo pesa au Mix by Yas, M-pesa, Airtel Money, Azam Pesa nk.

Sasa akataka kufahamu ikiwa pia mifumo iliyoelezwa kwenye kitabu ingeweza ikatumika na huko pia. Kimsingi nilimjibu ndiyo inawezekana ijapokuwa biashara ya miamala ni tofauti kidogo kwani hushughuliki na stoku ya bidhaa bali fedha taslimu na kwa kadiri fedha zilivyokuwa nyeti basi inahitaji usimamizi wa kipekee zaidi hasa kwa yule utakayemwachia biashara mfano kutokumwachia akae na fedha taslimu mkononi kwa muda mrefu zaidi ya siku moja  kuepuka vishawishi vya kudokoa.

Katika makala yangu nyingine moja ya ushauri kwa mwanafunzi anayetaka kuanzisha biashara akiwa bado anasoma isemayo;-Biashara & uwekezaji mwanafuzi anaweza kuanza akiwa chuo, kidato cha 5, 1, darasa la 1 hata chekechea kuna mahali nilitoa ushauri huu ufuatao;-

“Kama  ni lazima mwanafunzi ufanye biashara, basi wekeza katika miradi isiyohitaji sana muda na uwepo wako pale lakini pia epukana na miradi yenye hatari kubwa”

Mwishoni Katarina alikata shauri ya kubaki kwenye biashara ya nguo shauri ya hatarai nyingi tulizoziona kwenye biashara ya miamala ya simu kwa mazingira yake binafsi na siyo kama haiwezekani kabisa hapana.

Katarina hakuishia hapo alikuja kunipigia tena simu mara ya tatu na safari hii aliniambia ya kuwa alikuwa amewasiliana na jamaa yake mwingine wa karibu ambaye naye anamiliki biashara ya duka la kuuza nguo rejareja jijini Mwanza.

Huyu jamaa yeye licha ya kumtajia mpaka eneo zuri la kuanzisha hii biashara, alimshauri pia biashara akaifungue Mwanza mjini kuliko na mzunguko mkubwa wa watu badala ya eneo la awalii alilokuwa amepanga ambalo ni kijijini (Wilayani) japo pamechangamka kidogo na panafanyika minada ya vitu mara 2 kwa wiki.

Nilimuuliza maswali machache mojawapo likiwa ni ikiwa huyo mshauri mwingine ana maslahi yeyote binafsi anayoweza kuwa anayalenga kutoka kwake pengine ya kifedha kiuhsiano wa mapenzi au hata ikiwa ni dalali. Lakini majibu yake yalinidhihiririshia pasi na shaka kuwa ‘mentor’ huyo hakuwa na maslahi yeyote mengine yaliyojificha zaidi tu ya kutaka msichana huyu aweze kutimiza dhamira/malengo yake ya kumiliki biashara ya nguo akiwa bado anasoma

Basi ndipo na mimi nilipoungana na yule mshauri namba 2 na kumwambia Katarina kuwa ikiwa upo uwezekano wa biashara hiyo kuanzishwa mjini, hakuna sababu ya msingi akaifungulie kijijini licha ya wasiwasi wake mkubwa kwamba eti kodi ya pango la fremu ya biashara mjini ilikuwa ni shilingi milioni mbili kwa mwaka kiasi ambacho ni kikubwa mno. Nikamtia moyo kwamba kodi ya pango  kubwa lakini pakiwa na mzunguko mkubwa wa biashara siyo ishu (tatizo)

Nilimsihi kitu cha kwanza afanye utafiti wa soko mahali hapo huyu mshauri alipomwelekeza kujiridhisha ikiwa kama kweli pana wateja na biashara itaweza kutoka vizuri, achunguze na biashara za wengine kama yakwake (washindani wake watarajiwa) mauzo yao yanaweza kufika shilingi ngapi kwa siku nk.

Kulingana na lengo lake la kuwa na biashara inayozunguka chapchap ili iweze kumudu gharama za kumlipa mfanyakazi huku na yeye akipata faida nilimwambia aachane na wazo la kwenda kufungua biashara hii kijijini kwa madai ya gharama kuwa kidogo kwani itamchelewesha.

Midhali mtaji aliniambia anao wa kutosha kulipia kodi ya fremu hata ya miezi sita na kiasi kingine kubaki kwa ajili ya kununulia bidhaa za nguo, usajili wa TIN namba na leseni ya biashara, nilimwambia maneno yafuatayo,

“Jitoe mhanga kachukue hiyo fremu ufanye biashara, huwezi kufanikiwa pasipo ‘kutake risk’ ila hakikisha hakuna mazingira yeyote yale ya utapeli yanayoweza kuwepo baina yako na yule mshauri uliyeniambia amekutafutia eneo la kufanyia biashara”    

Nilimwambia Katarina pia kwamba mbinu na mifumo aliyojifunza kwenye kile kitabu cha MAFANIKIO YA BIASHARA YA DUKA LA REJAREJA 2025 & GENGE NDANI YAKE  hususani ule mfumo wa kudhibiti mapato yasiibiwe hata shilingi na msaidizi utafanya kazi kwa ufanisi zaidi endapo tu “turn over” ya biashara ni kubwa nikimaanisha kwamba mzigo unaisha chapchap na kwenda kununua mwingine haraka jambo linalosababisha faida kuongezeka upesi (good ROI) na kufanya gharama zilizotumika kuanzisha biashara kurudi kwa kipindi kifupi sana kijacho kabla hata hajamaliza chuo (short break even point)

Habari hii kuhusiana na safari ya Msichana Mwanafunzi wa chuo Kikuu anayetaka kumiliki biashara angali bado chuoni akisoma haijaishia hapa kwani ndio kwanza anafanya utafiti kusudi aje aanze.

Nakuahidi nitakupa mrejesho (Updates) kadiri mambo yatakavyokuwa yakiendelea na hata ikibidi uje ufahamu ikiwa kama alifanikiwa ama la, kwani kwa jinsi nijuavyo mimi tabia za wanafunzi wa chuo, Katarina hataishia pale aliponiuliza mara ya pili na ya tatu, atarudi tena na tena kuniuliza mambo mengine mengi na mimi nimejiandaa kumpatia majibu ya kina yatakayomsaidia kwenye safari yake hii muhimu kabisa maishani ya kumiliki uchumi wake mwenyewe.

 

Makala hii imeandaliwa na

Peter Augustino Tarimo

Whatsap/Call: 0765553030

 

 

SOMA NA HIZI HAPA PIA;

1.     Kuanzisha biashara nikiwa chuoni nasoma nipeni ushauri nina wakati mgumu

2.     Ushauri kwa mwanafunzi aliyehitimu chuo/masomo anayetaka kuanza

3.     Biashara nzuri 4 mwanachuo anaweza kufanya na mtaji wa laki 2 huku akisoma

4.     Msomi chuo kikuu, UDSM amiliki biashara yake

5.     Biashara ya laini na miamala ya simu kwa mwanafunzi wa chuo kikuu, mtaji laki 3 –ushauri

6.     Biashara & uwekezaji mwanafuzi anaweza kuanza akiwa chuo, kidato cha 5, 1, darasa la 1 hata chekechea

7.     Biashara ndogondogo zenye faida ya haraka tanzania ni hizi hapa, zipo nne(4)

8.     Kijana mwenye malengo makubwa kiuchumi: nifuge kuku aina gani, mayai, nyama au kienyeji? nishauri tafadhali

9.     Biashara 7 nzuri za kufanya zitakazokuingizia pesa hata kama umelala

10. Somo:mamilionea vijana 10 wakisimulia siri za utajiri wao walivyofanikiwa

 

0 Response to "ENEO LA BIASHARA YA DUKA LA NGUO REJAREJA, JE NIFUNGUE MJINI AU KIJIJINI?-MWANAFUNZI WA KIKE CHUO KIKUU"

Post a Comment